TAFADHALI MAMA USIWAUE WATOTO WANGU 28-----29


“Hapana sihitaji kufanya haraka sana, nahitaji kujua mambo mengi zaidi juu ya huyu mtu!” Aliwaza Patrick akilielekea jukwaa na kuamua kunyamaza kimya juu ya mambo aliyoyaona.
Baada ya mahubiri mjini Mbeya safari iliendelea kwenda Malawi, Msumbiji, Zambia, Zimbabwe na hatimaye Afrika ya Kusini, kote huko mizigo ya madawa ya kulevya ikiendelea kumiminwa ikipelekwa kama misaada kwa watu wasiojiweza katika nchi ambazo Mwinjilisti Heinz alihubiri.
Jambo hilo Patrick alilielewa na kuamua kufunga na kumwomba Mungu ambadilishe Mwinjilisti Heinz kwani idadi kubwa ya watu walizidi kuharibika.Maombi yake yalisikika na Mungu akaamua kumpa Mwinjilisiti Heinz pigo ili amnyanyue Patrick! Wakiwa nchini Afrika ya kusini mizigo ya Mwinjilisti Heinz ilikamatwa na kugundulika ilikuwa ni madawa ya kulevya lakini kabla yeye hajakamatwa alitoroka na siku iliyofuata alikutwa akiwa amegogwa na treni iliyokuwa ikielekea Soweto.
Pembeni mwa maiti yake iliyogawanywa vipandevipande ilikuwepo barua ndogo iliyoeleza ni kwanini alifikia uamuzi huo na aliwaomba msamaha kwa watu wote aliowaharibu kwa kuwaonjesha madawa ya kulevya na kuwafanya wawe watumiaji!Watu wengi katika nchi alizopita tayarii walikuwa walevi wa madawa ya kulevya kupindukia.
Dunia nzima ilishtushwa na habari ya kifo cha mwinjilisti Heinz na kukamatwa kwa madawa ya kulevya! Shirika la Global outreach lilipigwa mafuruku kujihusisha na kazi ya Mungu!
Kwa sababu Patrick alimpenda Mungu na alitaka kuendelea kuifanya kazi yake akiwa nchini Afrika ya Kusini aliamua kuingia katika chuo cha Uinjilisti, chuo hicho kilimilikiwa na dhehebu la Kibaptisti, alisoma kwa miaka mitatu akiamini Mungu alikuwa na mpango wa kumtumia.
Alipomaliza masomo yake kwa msaada wa Thabo Nhblala, tajiri mmoja nchini Afrika ya Kusini aliyemtegemea Mungu katika kila kitu na alitamani kutumia mali zake kueneza neno la Mungu, Patrick alianzisha shirika lake lililoitwa Bring souls to Jesus inc.Kazi ya shirika hilo haikuwa tofauti na kazi iliyofanywa na shirika la Mwinjilisti Heinz.
Kwa umaarufu alioupata akiwa na Heinz haikuchukua muda mrefu sana Patrick akawa amejulikana sana nchini Afrika ya Kusini na nchi zote za jirani, kuingiza huduma yake katika mtandao wa Internet ilimfanya ajulikane zaidi na kupata mialiko mingi kila mahali, watu wote walimtambua kwa jina la Patrick Heinz sababu ya Mwinjilisti aliyefanya naye kazi.
Alikuwa kijana mdogo lakini miujiza aliyoifanya kwa jina la Yesu ilikuwa mikubwa mno! Mwanzoni watu hawakuamini wengi walifikiri alifanya mchezo kama wa Heinz lakini alipochunguzwa alikutwa ni safi.
Watu wengi wenye magonjwa mbalimbali walipona, wenye mapepo na mikosi walifunguliwa na kufanya watu kufurika katika kila mkutano aliohubiri. Katika kipindi cha miaka minne ya huduma yake tayari alishatembelea nchi za Ujerumani, Hispania, Canada, Marekani na alikuwa njiani kuelekea Uingereza alikoalikwa na Wakristo wa huko.
Kwa miujiza aliyoifanya sifa zake tayari zilishaenea dunia nzima nchini Uingereza watu waliusubiri ujio wake kwa hamu kubwa!Makanisa yote yalijiandaa kwa mkutano huo mkubwa aliotarajiwa kuufanya katika jiji la London Septemba 23,2000.
*****
Septemba 22, 2000 mvua kubwa ilikuwa ikinyesha katika jiji la London, watu wengi walishangazwa na mvua hiyo kwani haikuwa kawaida, walivaa makoti makubwa kujikinga na baridi, Nancy na mumewe walikuwa wakiteremka ndani ya ndege ya KLM wakitokea Tanzania walikokwenda kumchukua Anne baada ya kupata msamaha wa Rais!
“Mama hii ndiyo London karibu sana!”
“Ahsante sana mwanangu siamini macho yangu kumbe nilifanya vizuri nilipokuruhusu uondoke kuja huku, nami leo nimepanda ndege kweli Mungu ni mkubwa !” Alisema Anne.
Pamoja na kuvaa nguo nzuri bado mwili wake ulionekana kuwa na ukurutu,alionyesha wazi afya yake haikuwa nzuri!Nguo zake zililoa kwa damu, njiani walilazimika kumbadilisha nguo mara mbili! Nancy alikaa na pafyumu kali aliyompulizia mama yake mara kwa mara kuzuia harufu aliyohofia ingewasumbua abiria wengine ndani ya ndege hiyo.
“Nakutesa mwanangu?”
“Hapana mama najua yote haya yalikupata sababu yangu mimi na Patrick kaka yangu!”
Waliongea mengi wakiwa ndani ya gari kuelekea nyumbani kwao, dereva alifungulia redio 120fm iliyokuwa ikirusha matangazo ya dini, redio hiyo ilimilikiwa na kanisa la Kibaptisti. Mtangazaji alitumia muda mrefu sana kuongea habari za mkutano wa injili uliokuwa utikise jiji la London siku iliyofuata na alitaja wazi kuwa mkutano huo ungehubiriwa na Mwinjilisti wa Kimataifa Patrick Heinz wenye magonjwa mbalimbali waliombwa kuhudhuria.
“Patrick!Jina kama la marehemu mwanangu!” Alisema Anne na kuanza kulia mpaka wakati huo Nancy alikuwa hajamwambia kuwa aliwahi kumwona Patrick jijini Dar es Salaam, aliifanya hiyo siri kwa sababu hakuwa na uhakika kama kweli aliyemwona alikuwa ni Patrick labda kama angekutanana naye ana kwa ana.
“Usijali mama ulikuwa mpango wa Mungu!”
“Hakuna shida lakini naomba sana kesho mnipeleke kwenye huo mkutano nikaombewe labda nami naweza kupona nimeteseka muda mrefu mno na nina hakika haya ni mapepo!”
“Sawa mama!”
*****
Maelfu ya watu walifurika katika viwanja vya London City Gardens wakimsikiliza mtumishi wa Mungu Patrick Heinz, wengi walikwenda ili kushuhudia mwafrika akifanya miujiza, lilikuwa si jambo rahisi kuamini walipoambiwa kuwa viwete walitembea na vipofu waliona kwa uwezo wa Mungu.
“There is woman a amidst you! This woman has been suffering for a longtime, she has been bleeding for years to an extent that she lost hope! But today she is gonna be delivered form all the bounds the Devil! Please come forward!(Kuna mwanamke kati yenu, mwanamke huyo ameteseka kwa muda mrefu sana, amekuwa akipata hedhi kwa miaka mingi kiasi cha kupoteza matumaini, lakini leo anakwenda kufunguliwa na kuwekwa huru na kamba zote za shetani tafadhali mama huyo apite mbele! Bwana asifiwe sana!”
Watu wote waliitikia ameeni kisha wakabaki kimya wakiangalia ni mwanamke gani angepita mbele baada ya Mwinjilisti Patrick Heinz kusema maneno hayo.
Patrick aliyekuwa na miwani myeusi usoni aliangaza macho yake huku na kule katikati ya umati mkubwa wa watu waliokuwepo uwanjani!
“Please come forward! I know you’re there, don’t afraid Jesus is gonna set you free from all the sufferings, come!come forward!”(Tafadhali njoo mbele, ninajua upo, usiogope kwa sababu Yesu anakwenda kukufungua kutoka katika maumivu yote uliyonayo! Njoo! Njoo mbele!) Aliendelea kusema Patrick huku akiangaza macho yake kila upande wa mkutano, sauti ilikuwa imemwambia moyoni mwake kuwa palikuwa na mwanamke mwenye matatizo hayo katikati ya watu.
“Nancy kweli twende mbele mwanangu?”
“Twende tu mama na wala usiogope!” Alijibu Nancy na yeye pamoja na mumewe walianza kumsaidia Anne kusimama wima kisha wakaanza kutembea taratibu kwenda jukwaani.
****
Makumi kwa maelfu ya watu walikuwepo katika viwanja vya London City garden kumsikiliza Mwinjilisti wa Kimataifa Patrick Heinz, nyimbo nzuri za mapambio zilisikika kila mahali katika mkutano huo, watu wengi walisikika wakilia na wengine walionekana wakianguka chini na kutupa miguu na mikono yao huku na kule hewani mapovu yakiwatoka mdomoni!
Mapepo yalikuwa yakitoka yenyewe sababu ya uwepo wa Mungu maeneo hayo! Vilema walikuwa wakitupa magongo yao na kutembea kwa uwezo wa Mungu! Jina la Yesu lilitajwa kila mahali viwanjani hapo, ilikuwa ni miujiza ya ajabu ambayo hata siku moja Nancy, Smith, Anne na wananchi wengine wa Uingereza hawakuwahi kuishuhudia.
Miujiza yote hiyo haikumtosha Patrick aliyekuwa amesimama jukwaani akihubiri neno la Mungu, bado aliendelea kupaza sauti yake kwa kipaza sauti akimwomba mama aliyekuwa na matatizo ya kutokwa na damu kwa miaka mingi ajitokeze mbele upesi!
“Please come forward, don’t afraid of anything! Because today is the last day of your toutures, Jesus Is going to set you free!My late mom suffered the same kind of disease she died many years ago, because she had no chance to meet the power of God! Come forward and receive healing ! I’m not leaving this place untill I see you!”(Tafadhali mama njoo mbele usiogope kitu, leo ndiyo siku ya mwisho ya mateso yako! Yesu anakwenda kukufungulia, mama yangu pia aliwahi kupatwa na ugonjwa kama unaokusumbua wewe, alikufa miaka mingi iliyopita kabla hajakutana na nguvu za Mungu, njoo mbele upokee uponyaji!) Patrick alizidi kupaza sauti yake hewani kwa nguvu zake zote akimwomba mama huyo apite mbele! Ndani ya moyo wake alisikia msukumo wa ajabu na alitaka sana kumsaidia mama huyo aliyeteseka kwa muda mrefu!
Ghafla akiwa juu jukwaani alimwona mwanamke mmoja akipita katikati ya watu kuelekea jukwaani, alikuwa ameshikwa na watu wawili msichana mmoja wa Kiafrika upande wa kushoto na mzee wa Kizungu upande wa kulia! Ndani ya moyo wake alisikia sauti ikimwambia “Ndiyo huyo” Aliamini hiyo ndiyo ilikuwa sauti ya Mungu.
Mwanamke huyo alipandishwa jukwaani, alipomwangalia vizuri usoni aligundua mama huyo alikuwa akilia machozi na hata msichana aliyekuwa naye pia alikuwa akibubujikwa na machozi kwa wingi.Nguo zote za mama huyo zililowa damu na mwili wake ulionekana mweupe sababu ya kupungukiwa damu na ulichakaa akawa kama mzee.
“Usiwe na wasiwasi mama! Mungu anakwenda kukufungua!” Alisema Patrick kwa sauti ya upole akimgusa mama huyo begani.
Patrick hakuwa na wasiwasi sababu alijua siku hiyo ndiyo ilikuwa mwisho wa tatizo la mama huyo.
“Mwachieni tu!”Patrick aliwaeleza msichana na mzee wa Kizungu waliomshika mama huyo pande zote.
“Mama unaitwa nani?”
“Naitwa Anne!”
“Anne??????” Patrick aliuliza kwa mshangao, jina hilo na tatizo alilokuwa nalo mama huyo yalimkumbusha matatizo aliyowahi kuwa nayo marehemu mama yake! Alishindwa kuamini alichokisikia ikabidi avue miwani yake ili amwone vizuri.
“Ulianza lini kupatwa na tatizo hili?”
“Miaka mingi sana iliyopita nikiwa msichana mdogo!”
“Nini kilikuwa chanzo!”
“Nilirogwa na mama yangu mzazi huko Tanzania!”
“Mh!”Patrick aliguna aliposikia neno Tanzania, alipomwangalia kwa makini zaidi mama huyo na baadaye kutupa macho yake upande wa pili kumwangalia msichana aliyekuwa jirani yake, Patrick alijikuta akiruka na kuwakumbatia wote wawili na wote watatu wakaanguka chini! Viongozi wa kanisa walishangazwa na kitendo hicho, wakafikiri labda mwinjilisti Patrick alipatwa na tatizo fulani, wote walinyanyuka na kukimbia hadi sehemu waliyoangukia.
“What is up Evangelist?”(Nini kimetokea Mwinjilisti?”
“My mom! My mom and my sister! I knew they were all dead!(Mama yangu! Mama yangu na dada yangu! nilijua wote ni wafu) Alipiga kelele Patrick na maneno hayo yalimfikia Nancy moja kwa moja naye alipomwangalia Patrick usoni aligundua ni kaka yake aliyemtafuta Dar es Salaam miaka mingi kabla baada yakumwona akihubiri jangwani.
“Hey Pat! Ni wewe?”Alianza kulia kwa furaha Nancy, mzee Smith alibaki pale ameduwaa bila kujua la kufanya, alishangaa kila kitu kilichoendelea wote watatu Patrick, Nancy na Anne walikuwa wakilia machozi ya furaha!
Baadaye Patrick alinyanyuka na kusimama wima nyuma yake wakiwa wamesimama viongozi wa kanisa, alikuwa mbele ya mama yake aliyelala chini akilia kwa furaha Patrick alianza kumwomba Mungu na kumkemea shetani.
“You the devil, who has tortured my mom for all those years, making her bleed like river nile! Today is your day, I command you in the name of Jesus my saviour get out of my mother’s body nooow! And go to hell! In the name of Jesus be burnt with fierce fire in the name of Jesus! Why did you make my mother a slave of your torments! Go! Go! Go to hell in the name of Jesus and never come back!”(We shetani, uliyemtesa mama yangu kwa miaka yote ukimfanya kutokwa na na damu kama mto nile, leo ndiyo siku yako, ninakuamuru katika jina la Yesu Mwokozi wangu toka katika mwili wa mama yangu sasa na uende jehanamu na usirudi tena! Katika jina la Yesu ungua na moto mkali kwanini ulimfanya mama yangu mtumwa wa mateso yako? Nenda!Nenda! Nenda jehanamu na usirudi tena) Jasho jingi lilikuwa likimtoka Patrick wakati akimwombea mama yake, machozi pia yalimtoka na kuzilowanisha nguo zake.
Alirukaruka kama mtu aliyechanganyikiwa wakati akisali jukwaani, watu wote walikuwa kimya wakimsikiliza yeye, Nancy alikuwa akilia machozi macho yake yakiwa yameelekeza sakafuni alipolala mama yake akihangaika na kutupa mikono na miguu huku na kule hewani, macho na ulimi wake ukiwa umetolewa nje!
Nancy alifikiri mama yake alikuwa akikata roho, alianguka juu yake na kuanza kulia lakini ghafla aliruka tena juu baada ya kuunguzwa na mwili wa mama yake uliokuwa na joto kali.
“Mama anaunguza kama moto!” Alipiga kelele baada ya kusimama.
“Mwache usimguse shetani sasa anateketea! Ameshindwa katika jina la Yesu!” Alisema Patrick.
Ghafla watu wote walishangazwa kuona kitu kama moshi mzito ukimtoka Anne mwilini na kupanda juu uka!Baada ya tukio hilo Anne akarejewa na fahamu zake na kuketi kitako sakafuni, alijisikia ana nguvu ya ajabu! Alisikia damu ikikatika kama mtu aliyefunga bomba! Hakujisikia unyonge tena mwilini mwake alisimama wima na kuruka juu akiimba wimbo wa kumsifu Mungu.
“At last I’m free, Praise the name of the Lord!” (Hatimaye nimewekwa huru jina la bwana lipewe sifa!)Alipiga kelele Anne, badala ya kuonekana kizee kama alivyokuwa alionekana kijana zaidi! Wakati wote huo watu uwanjani hapo waliitikia Haleluya!
“Haleluyaaaa!” Patrick alidaki na kuuliza watu.
“Ameeeni!”
“Today I’m extraordinarily happy because two things have happened in my life. One, I have seen my mom and my sister, whom I believe they were dead! Secondly, Jesus through me has healed my mom of the continuos bleeding she had! Praise the Lord!”(Leo nina furaha isiyo ya kawaida kwa sababu vitu viwili vimetokea katika maisha yangu.Cha kwanza, nimekutana na mama yangu pamoja na dada yangu, watu ambao niliamini walikufa! Cha pili, Yesu kwa kupitia kwangu amemponya mama yangu na ugonjwa wa kutokwa na damu uliomsumbua kwa miaka mingi! Bwana asifiwe sana!) Alisema Patrick huku akilia kwa furaha.
Mpaka wakati huo ilikuwa si rahisi hata kidogo kwa Patrick kuamini alikuwa amekutana na familia yake, yote yaliyotokea yalionekana kuwa ndoto zaidi kuliko hali halisi!
Machozi ya furaha yalizidi kumtoka Anne na alipojisikiliza vizuri kwa ndani hakuisikia damu ikitiririka kama ilivyofanya akaamini alikuwa ameponywa.
Anne alibaki amesimama akiwa amepigwa na butwaa, alihisi mwili wake kufa ganzi! Hakuamini kama aliyekuwa amemponya alikuwa mtoto wake mwenyewe waliyepoteza miaka mingi, ilikuwa si rahisi hata kidogo kuliamini jambo hilo.
“Patrick!”
“Naam mama!”
“Kweli ni wewe mwanangu?”
“Ni mimi mama!”
“Hebu nyanyua mkono wako wa kulia, nikuone kwapani!” alisema Anne kuna alama aliyokuwa nayo Patrick kwapani aliyoamini ingempa utambulisho sahihi.
Bila ubishi Patrick alifungua vifungo vya shati lake mbele za umati wa watu na kunyanyua mkono wake na mama yake akamchunguza kwapani, aliliona kovu kubwa ambalo Patrick alilipata baada ya kuungua na uji akiwa mtoto wa miaka miwili! Anne aliruka kwa furaha na kumkumbatia mtoto wake, Nancy naye aliungana nao na wote waliendelea kulia machozi ya furaha.
Watu mbalimbali waliokuwepo mbele walipiga picha za tukio hilo kama ukumbusho na mkutano wa siku hiyo ulifikia tamati! Watu walianza kusambaa kuelekea majumbani kwao, wengine wakiwa hawajaamini hata kidogo kama kweli Mwinjilisti Patrick ni siku hiyo ndiyo alikuwa amekutana na dada pamoja na mama yake!
Wakati wanateremka jukwaani Nancy alimshika Patrick begani akageuka na kumwangalia.
“Vipi dada?” Patrick aliuliza.
“Huyu hapa ni shemejio! Ndiye aliyenileta mimi hapa London anaitwa Mr Smith!” Nancy aliwatambulisha wote ili wafahamiane.
“Nice to meet you sir! Thanks for everything it is you who have made our meeting possible!”(Nafu
rahi kukutana na wewe bwana, ahsante kwa kila kitu ni wewe uliyefanikisha kukutana kwetu)
“Nice to meet you too! You are warmly welcome at our home!(Nimefurahi pia kukutana na wewe unakaribishwa sana nyumbani kwetu) mzee Smith alisema maneno hayo huku akitabasamu.
Gari la kumchukua Mwinjilist Patrick kumpeleka katika hoteli ya Sentimental aliyofikia lilikuwa tayari na lilisogezwa karibu kabisa na mahali aliposimama ili apande lakini hakufanya hivyo aliendelea na maongezi huku akiwa amemkumbatia mama yake!
“Mama inabidi tu nikuage ingawa sipendi kukuacha ningetaka tuwe siku zote kuanzia saa hii!”
“Nenda tu mwanangu kwa sababu una wenyeji wako!”
“Ulifika lini hapa Uingereza?”
“Nimefika jana tu!”
“Jana?”
“Ndiyo! Walinifuata baada ya kumaliza kifungo changu”
“Nancy!”
“Naam kaka!”
“Tafadhali kesho uje hotelini unichukue nije nyumbani kwenu tupate kuongea mengi yaliyojitokeza katika maisha yetu, mkutano wetu unakwisha kesho na baada ya hapo nitakaa na nyinyi kwa muda kabla sijarudi Afrika ya Kusini)
“Sawa kaka tuje saa ngapi?”
“Saa tatu na nusu nitakuwa tayari!” Alisema Patrick“
Mwinjilisti Patrick aliwabusu wote usoni na kuondoka ndani ya gari hadi hotelini ambako hakupata usingizi hata lepe, muda wote alimfikiria mama na dada yake na alimshukuru Mungu kwa kuwakutanisha nao tena.
**********************
Siku iliyofuata majira ya saa tatu asubuhi kengele ya simu ililia chumbani kwa Mwinjilisti Patrick aliyekuwa akijiiandaa kwa safari ya kwenda nyumbani kwa dada yake, kwa asilimia zaidi ya mia moja alijua simu ile ilitoka mapokezi kwa lengo la kumtaarifu kuwa waliokuja kumchukua walikuwa wakimsubiri.
Aliisogelea meza na kuichukua simu na kuanza kuongea.
“Hallo mwinjilisti Patrick hapa!”
“Ndiyo hapa ni mapokezi ,kuna mtu anakuhitaji!”
“Nani?”
“Ni mzee mmoja ana ndevu nyingi kama sikosei ni mzee Smith tajiri wa hapa London!”
“Oh! Sawa nakuja huyo ni shemeji yangu amemuoa dada ambaye ni pacha wangu!”
“Aisee! Basi yupo hapa wahi kama unaweza kuwahi!”
“Nipe dakika mbili!”
Patrick aliitengeneza tai yake vizuri na kuvaa koti juu ya shati lake la rangi ya kahawia kisha akachukua biblia yake ndogo aliyotembea nayo kila mahali alikokwenda na kuanza kushuka ngazi taratibu kuelekea mapokezi. Ni kweli mtu aliyekuwa akimsubiri hakuwa mwingine bali mzee Smith! Patrick alifurahi sana kumwona na kuonyesha tabasamu la wazi lakini badala ya mzee Smith kujibu kwa tabasamu alianza kulia machozi, moyo wa Patrick ulishtuka ghafla na mapigo yakaanza kwenda kwa kasi, alishindwa kuelewa ni kitu gani kilikuwa kimetokea!
“What is up Smith!?”(Nini kimetokea Smith) Aliuliza kwa mshangao.
“I’m very sorry to tell you this!”(Ninasikitika kukuambia haya!)
“What is it Smith?”(Ni nini unachotaka kuniambia?) Aliendelea kuuliza Patrick.
“We had a bad accident yesterday as we left the grounds! Our car collided face to face with another lorry! Your mom and Nancy are…………(Tulipata ajali mbaya jana tulipoondoka uwanjani kwenye mahubiri, gari yetu liligondana na gari jingine mama yako na Nancy wame...........
.)Alisema Mzee Smith huku akilia.
Whaaaaaat?What has happened?(Niniiiiiiiiii? Nini kimetokea?)
Badala ya kujibu swali hilo mzee Smith aliendelea kulia machozi na kufanya Mwinjilisti Patrick azidi kuchanganyikiwa, hakutaka kabisa kukubali kuwa Nancy na mama yake walikufa katika ajali hiyo kama jinsi akili yake ilivyomwambia.
“Inawezekanaje niwaone kwa siku moja tu halafu wafe? Hakuna hii haiwezekani! Alipiga kelele Patrick huku akilia.
Je, Nancy na mama yake wamekufa?
Na je, nini kitamtokea Patrick nchini Uingereza?
Kazi ya Mungu itasonga mbele?
Na nini kiliwapata Suzanne na Anorld gerezani? Mwinjilisti Aaron je?
Kwa kuwa ni mwaka mpya umeingia, 


HADITHI: TAFADHALI MAMA USIWAUE WATOTO WANGU 29
MTUNZI: ERIC JAMES SHIGONGO
“Wamekuwa niniii?” Patrick aliuliza kwa mshangao mkubwa huku machozi yakimtoka, hakutaka kabisa kuamini kuwa Nancy na mama yake Anne walikuwa wamekufa! Mzee Smith hakujibu kitu zaidi ya kuendelea kububujikwa na machozi.
“Wewe niambie tu! Hata kama wamekufa usiogope!”
“Hawa.....ja...fa! Ila hali zao ni mba..ya sa..na hawa..we..zi kuongea”
“Wako wapi?”
“Wako chumba cha wagonjwa mahututi hospitali ya rufaa ya London!”
“Twende!” Alisema Patrick na wote walitoka wakikimbia hadi nje ambako waliingia ndani ya gari la mzee Smith na kuondoka kwa kasi kuelekea hospitali! Ulikuwa ni mwendo wa kama dakika ishirini kufika hospitali lakini walitumia dakika sita, gari lilipoegeshwa waliteremka na kuanza kukimbia kwenda chumba cha wagonjwa mahututi mzee Smith alisahau hata kufunga mlango wa gari lake.
“Jamani mnakwenda wapi?” Aliuliza muuguzi aliyekuwa ofisini wakati Patrick na mzee Smith wakiingia chumba cha wagonjwa mahututi.
“Ah!Tunakwenda kuwaona wagonjwa wetu!”
“Lakini huo sio utaratibu wetu hiki ni chumba cha wagonjwa mahututi kinahitaji utulivu mkubwa!”
“Wagonjwa wenu majina yao ni yapi?”Alisema muuguzi akifungua kwenye daftari lililokuwa mezani.
“Ni Nancy na Anne!”
“Ah! Hao wamepelekwa chumba cha upasuaji!”
“Hali zao?”
“Kwa kweli hali zao sio nzuri sana lakini matumaini yapo!”
“Katika Jina la Yesu nguvu za kifo zimeshindwa!” Patrick alitamka maneno hayo baada ya muuguzi kukamilisha sentensi yake.
“Njooni msubiri hapa nje muda si mrefu watatoka chumba cha upasuaji!”
Patrick huku akiwa na maumivu makali moyoni, maumivu ya kukutana na mama pamoja na dada yake kwa muda mfupi baada ya kupotezana kwa miaka mingi alitoka nje kwa unyonge na kwenda kukaa kwenye kiti kilichokuwa nje ya wodi, muda mfupi baadaye alipiga magoti na kuanza kumwomba Mungu awaongoze madaktari wote waliokuwa wakiwafanyia operesheni mama na dada yake.
Ikawa nusu saa, mwisho saa nzima hatimaye masaa matano bila Nancy na Anne kurudishwa wodini kutoka chumba cha upasuaji, moyoni mwa Patrick tayari wasiwasi kuwa ndugu zake walikuwa maiti ulimtawala, alijua walikuwa wamefia juu ya vitanda vya operesheni lakini wauguzi hawakuwa tayari kuelezea ukweli!
Mawazo kama hayo pia yalimsumbua mzee Smith kichwani mwake na kumfanya aendelee kulia zaidi.
“I need to know the truth!”(Nahitaji kuufahamu ukweli!)
“That’s right!”(Hiyo ni sawa!)Aliitikia Patrick na wote wakanyanyuka na kuanza kutembea kuelekea mlangoni ambako waligonga kengele na muuguzi akatoka.
“Can I help you?”(Naweza kuwasaidia?)
“We need to know where is the operating Theater!”(Tunahitaji kujua mahali kilipo chumba cha upasuaji!)
“Why?”(Kwanini?)
“We just want to know!”(Tunataka tu kujua!)
“Ok! Go straight at that junction turn right you will see a room labelled OPT, that will be the operating Theater!”(Sawa! Nendeni moja kwa moja pale zinapokutana njia kateni kulia mtaona kibao kimeandikwa OPT hapo ndio chumba cha upasuaji kilipo!)
Patrick na mzee Smith wakiwa wamejawa na wasiwasi mwingi mioyoni mwao walianza kutembea kufuata maelekezo waliyopewa lakini kabla hawajakifikia chumba walichoelekezwa mlango ulifunguliwa na machela mbili zilitolewa, watu walikuwa juu yake wakiwa wamefunikwa mashuka meupe!Chupa za maji yaliyotiririka kuingia katika mishipa zilionekana kuning’inia na maji yalikuwa yakidondoka taratibu.
Hiyo peke yake ilitosha kuwaonyesha kuwa Nancy na Anne walikuwa wazima,Patrick alilitukuza jina la Bwana! Mzee Smith naye alionekana kutabasamu kwa furaha.
Machela ziliwapita na waliendelea kutembea wakizifuata kwa nyuma kuelekea wodini, hakuna mtu kati yao aliyekuwa na uhakika kuwa watu waliokuwa juu ya machela hizo walikuwa ni Nancy na Anne!Ilibidi mzee Smith akimbie mbio na kumgusa mmoja wa wauguzi begani.
“Are those patients Anne and Nancy?”(Hawa wagonjwa ni Anne na Nancy?)
“No!”(Hapana!)
“My God!”(Mungu wangu!) Mzee Smith alisema kwa sauti na kumfanya Patrick ashtuke na kwenda mbio hadi mahali aliposimama mzee Smith akiwa amejishika mikono kichwani, furaha yote iliyojitokeza iliyeyuka na kumfanya aanze kulia tena! Patrick aligundua ni kiasi gani mzee huyo alimpenda dada yake.
“What?”(Nini?)
“They are not!”(Sio wenyewe!)
“Sure?”(Una uhakika?)
“Yeah! Because the nurse told me!”(Ndiyo kwa sababu muuguzi ameniambia!)
“So what do we do?”(Sasa tufanye nini?)
“Go back to the Theater and wait!”(Turudi chumba cha upasuaji tusubiri)
Waliondoka na kutembea hadi chumba cha upasuaji, dakika tano baadaye milango ilifunguliwa tena na machela mbili zikatolewa kitu cha kwanza walichofanya kabla ya kufurahi ni kusogea karibu na kuangalia sura za watu waliolazwa juu ya machela hizo, ilikuwa si rahisi kuwatambua kwa sababu sura zao zilifunikwa na bendeji.
“Hawa ni akina Anne na Nancy?” Patrick alimuuliza muuguzi aliyekuwa akisukuma machela.
“Ndiyo! Nyie ni ndugu zao?”
“Mimi ni kaka yake na Nancy na mtoto wa huyu mama mwingine! Lakini huyu niliyenaye ni mume wa Nancy!”
“Lakini huyu namfahamu si ni tajiri Smith?”
“Ndiyo!”
“Hali zao si mbaya! Operesheni imechukua muda mrefu kwa sababu ya kurekebisha mifupa yao iliyokuwa imevunjika! Waliumia sana kwa kweli!”
“Watapona kweli?”
“Watapona wala msiwe na wasiwasi!”
Jibu hilo lilimfanya Patrick afurahi kupita kiasi ndani ya nafsi yake na hata mzee Smith naye alionyesha meno yake, machela zilisukumwa hadi chumba cha wagonjwa mahututi ambako vitanda viliandaliwa tayari kwa ajili ya Anne na Nancy.
******************
Kwa siku tano nzima Nancy na Anne walilala bila kujitambua, ulikuwa ni muda wa wasiwasi mkubwa kwa mzee Smith na Patrick, walisubiri kwa hamu kuona wakifumbua macho na kuongea nao, siku ya sita wote walizinduka usingizini kwa tofauti ya dakika arobaini na tano kati yao! Wa kwanza kuzinduka alikuwa Nancy.
“AMEFUMBUA MACHO!AMEFUMBUA MACHO NJOONI MUONE!” Alipiga kelele huku akirukaruka Mwinjilisti Patrick ambaye kwa siku zote tano alikaa hospitali pamoja na mzee Smith shughuli zote za mikutano alizisimamisha.
“Kweli?” Aliuliza mzee Smith na kusogea hadi pembeni mwa kitanda hakuamini macho yake alipomwona Nancy akiangaza huku na kule chumbani na baadaye kutabasamu, mzee Smith alipiga magoti na kumshukuru Mungu, kwa hali ilivyokuwa hakutegemea kama mke wake angeweza kupona.
Muda mfupi baadaye Anne alifumbua macho hivyohivyo na kufanya furaha iwe kubwa zaidi, hakuna aliyekuwa tayari kuamini kuwa watu hawa walikuwa wamerudi tena duniani.
“Huu ni kama ufufuo!” Alisema Patrick.
****************
Hali zao ziliendelea vizuri lakini walikaa hospitali kwa muda wa miezi sita ndio wakapona kabisa na kuruhusiwa kutoka hospitali! Operesheni zao zilifanywa vizuri sana kwani hawakubaki hata na kovu moja usoni.
Sherehe aliyoifanya mzee Smith kufuatia kupona kwa Nancy na Anne ilikuwa si ya kawaida! Watu wengi walihudhuria wakala na kunywa mpaka kusaza, ilikuwa ni furaha kubwa mno kwa Nancy mwenyewe ambaye alishajihesabu mfu! Lakini furaha zaidi ilikuwa ni kukutana kwa watu watatu waliopotezana kwa miaka mingi, katika muda wote wa sherehe hiyo Patrick alikaa pembeni mwa mama yake akiongea naye na kumpa pole ya matatizo yote yaliyomkumba katika maisha yake.
“Pole sana mama! Namshukuru Mungu tumekutana tena, mpaka sasa hivi siamini kama kweli wewe na dada yangu mpo hai!”
“Usijali mwanangu ila maisha yangu yalikuwa ya mateso mno!”
“Hilo nalijua mama ila yote yamepita ninaamini katika jina la Yesu hautateseka tena!”
“Kweli umetimiza ndoto yako mwanangu!”
“Ndoto gani mama?”
“Siku zote ulitaka kuwa mtumishi wa Mungu na kweli umekuwa!Mwanangu umeniponyesha na kuniondolea mateso yote niliyoyapata kwa miaka mingi!”
“Ni Mungu aliyefanya kazi hiyo mama! Yalikuwa ni mapenzi ya Mungu tupotezane na baadaye tukutane, nakupenda mama na nitaendelea kukupenda siku zote!” Alisema Patrick.
*************
Mwaka mmoja baadaye:
Mwinjilisti Patrick hakuondoka tena Uingereza, aliendelea kumtumikia Mungu katika nchi hiyo akihubiri kutoka mji mmoja hadi mwingine na kote alikopita alifungua makanisa na Waingereza wengi wakiwemo mzee Smith na mke wake Nancy waliokoka na kurejea kwa Kristo! Walimpa Patrick moja ya nyumba zao iliyokuwa katika mji wa Chelsea ambako aliishi wakati akifanya shughuli zake za kuhubiri neno la Mungu.
Maisha baada ya hapo yaliendelea kuwa mazuri lakini afya ya mzee Smith ndiyo iliendelea kubadilika, aliongezeka uzito kupita kiasi na madaktari walimshauri afanye mazoezi ili kujiepusha na ugonjwa wa shambulio la moyo uliowaua Waingereza wengi wakati huo.
Mazoezi hakikuwa kitu rahisi kufanywa na mzee Smith na hata kuepuka chakula cha mafuta pia ilikuwa ni kazi ngumu sana kwake, mzee huyo alipenda sana kula chakula cha mafuta na wanga vilivyomfanya azidi kunenepeana, alianza kupatwa na tatizo la kuhema kwa shida na maumivu makali sana kifuani na begani mkono wa kushoto.
“This is probably angina pectoris because of too much fat deposted onto the walls of your blood vessels!”(Nafikiri huu ni ugonjwa unaosababishwa na mafuta mengi kuganda kwenye kuta za mishipa ya damu na kuiziba!) Alisema Dk.Watson bingwa wa magonjwa ya moyo aliyemtibu mzee Smith, alikuwa na wasiwasi mkubwa kuwa mzee Smith angeweza kupatwa na ugonjwa wa shambulio la moyo au heart attack ulivyoitwa kitaalam.
*****************
Ilikuwa ni jioni ya siku ya Jumapili Nancy,Anne na mzee Smith wakiwa wamepumzika sebuleni wakisikiza nyimbo za dini,mzee Smith aliondoka sebuleni kuelekea chooni kujisaidia! Kila mtu alijua angerudi mapema lakini alichukua saa nzima bila kuonekana.
Nancy alifikiri labda mumewe aliamua kujipumzisha kitandani baada ya kutoka chooni, alimuaga mama na kwenda moja kwa moja hadi chumbani lakini hakumkuta! Moyo wake ulishtuka wazo la kwenda chooni kumwangalia halikumwijia mara moja, alitoka hadi nje na kuzunguka nyuma ya nyumba na kwenda hadi bustanini akifikiri mzee Smith alikuwa huko lakini hakumwona! Wasiwasi mkubwa zaidi ulizidi kumwingia ikabidi amtaarifu mama yake juu ya jambo hilo.
“Simwoni!”
“Chumbani?”
“Hayupo!”
“Kwani alipoondoka hapa alisema anakwenda wapi?”
“Aliniambia anakwenda chooni!”
“Umemwangalia chooni?”
“Hapana!”
“Hebu nenda kamwangalie basi!”
Nancy aliondoka na kurudi tena hadi chumbani kwao ambako alinyoosha moja kwa moja hadi chooni! Mama yake aliyekuwa sebuleni alichosikia baada ya hapo ni kilio na mayowe kutoka chumbani kwa mtoto wake.
“ Mama!Mamaa! Mamaa! Njoo uone! Ameanguka chini damu zinamtoka puani na masikioni!”
Anne hakutaka kupoteza muda alikimbia moja kwa moja hadi chumbani na baadaye kwenda hadi chooni, hakuamini alichokiona! Nancy alikuwa akijaribu kumtingisha mzee Smith aliyekuwa amelala chooni kichwa chake kikiwa karibu kabisa na tundu la choo! Damu nyingi ilikuwa ikitiririka kuingia katika shimo la choo.
“Nenda kampigie simu daktari upesi! Acha kulia kama mtoto mdogo!” Anne alimwambia Nancy huku akimvuta kutoka kwa mumewe.
Nancy alitii amri ya mama yake na kuondoka mbio hadi chumbani, alinyanyua simu na kumpigia Dk.Watson, daktari wao wa nyumbani ambaye alifika dakika kama tano baadaye na kumpima mbele ya Nancy na mama yake.
“I’m sorry....!”(Nasikitika....!)
“Sorry for what?”(Unasikitika nini?)
“Your husband is dead!”(Mume wako amefariki dunia!) Daktari alisema kwa sauti ya huzuni.
Nancy alianguka chini na kuanza kulia, sauti ya kilio chake iliwafikia majirani wengi kila mtu alisikitishwa na kifo cha mzee Smith! Mwili wake ulichukuliwa na kukimbizwa hospitali ambako ulihifadhiwa! Siku iliyofuata mazishi yaliyohudhuriwa na maelfu ya wakazi wa jiji la London yalifanyika, Kennedy mtoto pekee wa mzee Smith alikuwepo, aliwashangaza watu kwa jinsi alivyokuwa na moyo wa kishujaa! Hakulia machozi hata tone moja.
Wiki moja baadaye:
Kikao cha ukoo kilifanyika na iliamriwa mali ya marehemu igawanywe kwa watu wawili mbele ya mwanasheria wa familia, watu hao walikuwa ni mtoto Kennedy aliyepewa asilimia 55 na Nancy aliyepewa asilimia 45! Ilikuwa ni mali nyingi mno kwa Nancy kwani ilikadiriwa kuwa paundi za Kiingereza milioni mia moja hamsini sawa na shilingi za Kitanzania bilioni mia moja na hamsini!
Pamoja na kuhuzunishwa na kifo cha mumewe, Nancy akawa amebadilika na kuwa mwanamke tajiri! Hata yeye mwenyewe hakutegemea katika maisha yake kuwa siku moja angemiliki kiasi kikubwa namna hiyo cha pesa! Ilikuwa ni kama ndoto.
Baadhi ya ndugu wa marehemu Smith hawakuridhishwa na uamuzi huo, waliona Nancy hakustahili kupata kiasi hicho cha pesa,manung’uniko yalianza! Ni manung’uniko hayo ndiyo yalimfanya Nancy aamue kuuza kila kitu alichokuwa nacho kwa mnada na kuingiza pesa yote aliyoipata katika shirika la kaka yake Patrick ili zitumike kuhubiri Injili.
Watu wengi walishangazwa sana na uamuzi huo lakini kwa Nancy mwenyewe hilo lilikuwa ni jambo jema, aliamua kutoa kila alichokuwa nacho kwa ajili ya kazi ya Mungu na na aliamua kujifunza uimbaji wa upigaji wa kinanda ili amtumikie Mungu kwa nyimbo! Wote watatu waliondoka Uingereza na kuanza kusafiri kwenda sehemu mbalimbali duniani wakihubiri Injili na hatimaye kujikuta wakiwa Nairobi.
*******************
Hapakuwa kuwa na mkutano mkubwa kiasi hicho wa dini katika jiji la Nairobi, watu kutoka katika madhehebu mbalimbali walikusanyika kumsikiliza Mwinjilisti Patrick na mwimbaji wa kimataifa Nancy! Watu wengi walibadilishwa na mkutano huo na wengi waliponya magonjwa yao na mapepo yaliwatoka wengi.
Mkutano ulipomalizika Patrick alishuka jukwaani na kuanza kusalimiana na watu, ghafla macho yake yalitua usoni kwa mzee mmoja na macho yao yaligongana! Sura ya mzee huyo haikuwa ngeni machoni kwa Patrick ingawa kulikuwa na mabadiliko mengi sana usoni kwake, mzee huyo alivaa kama mtumishi wa Mungu.
“Mzee ni kama nakufananisha wewe ni nani hasa?”
“Hata wewe sura yako si ngeni kwangu! Ila sikumbuki vizuri mahali tulipokutana”
“Unaitwa nani mzee?”
“Ninaitwa Mchungaji Aaron ni Mtanzania nimeishi hapa Nairobi kwa miaka karibu ishirini nikimtumikia bwana!”
Patrick hakujiuliza mara mbili aliruka na kumkumbatia mzee huyo, jambo hilo liliwashangaza watu wengi wakiwemo mama na dada yake waliokuja mbio kutaka kujua nini kilikuwa kimemfurahisha Patrick kiasi hicho.
“Nini tena?”
“Mchungaji Aaron!Mchungaji Aaron! Nancy unamkumbuka mchungaji Aaron tuliyekaa kwake?”
“Ndiyo!”
“Huyu hapa nimemwona!”
Nancy alipiga magoti chini na kuanza kumwangalia mzee huyo, alikuwa ni yeye na alimkumbusha mambo mengi yaliyotokea maishani mwake! Wote watatu walinyanyuka na kusimama wima wakiwa wamemwangalia Anne aliyekuwa pembeni yao akilia machozi ya furaha, hakuamini kama alikuwa amekutana na mtu aliyewalea watoto wake yeye akiwa gerezani.
“Mchungaji ni wewe?”
“Ni mimi Anne siamini kama nimekuona, taarifa nilizozipata ni kwamba ulikufa ukiwa gerezani!”
“Nipo hai na Mungu ametukutanisha tena tunayo kila sababu ya kumshukuru! Mengi tutaongea baadaye! Mama yuko wapi?”
“Alifariki dunia miaka mitano iliyopita kwa ugonjwa wa Kisukari na presha!”
“Masikini!” Alijibu Anne kwa masikitiko.
Je, nini kitatokea?

Post a Comment

Previous Post Next Post